Mbeya. Wizara ya Mawasiliano na Uchukuzi imeombwa kupitia upya Sheria ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) iliyoanza kutumika Aprili Mwaka jana kwa madai kuwa ni kandamizi kwao ikiwa ni pamoja na ubovu wa mizani.
Mwenyekiti wa wamiliki na wasafirishaji wa mizigo na abiria Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, Elias Mwangine amesema hayo leo Novemba 2, 2021 kwenye kikao cha wadau wa usafirishaji kilicholenga kutoa elimu juu ya sheria ya udhibiti uzito ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016 na kanuni zake za mwaka 2018.
Mwanginde amesema kuwa baada ya sheria hiyo kupitishwa mwaka jana wamekuwa wakiumizwa sana kutokana na faini ya zaidi ya Sh500, 000 wanapobainika kuzidisha mizigo.
“Kimsingi sheria hii wakati inapitishwa wadau wa usafirishai hatukupata elimu ya kutosha hivyo imekuwa ni mwiba kwetu hivyo tunaomba Waziri mwenye dhamana kuliangali hilo kwa mapana na kubadilisha sheria hiyo”amesema.
Mwanginde amelalamikia ubovu wa baadhi ya mizani za Serikali akidai kuwa wanapotoka nchi za jirani zinaonyesha magari kutozidisha mizigo lakini wanapoingia Tanzania wanaelezwa kuwa na kosa hilo hivyo kuishauri Serikali kuzifanyia ukarabati wa mara kwa mara ili kuwasaidia wadau wa usafirishaji kuondokana na changamoto hiyo.
Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Juma Homera ameagiza wakala wa Barabara Tanzania (Tanroad) kwa kushirikiana na wakala wa vipimo kutoa elimu kwa watendaji wao katika maeneo ya mizani hususani madereva kuhusiana na matumizi ya sheria mpya ili kulinda barabara.

“Tanroads kuanzia sasa anzeni kutoa elimu kwa watu wa mizani na madereva kwani Serikali imetumia pesa nyingi kuboresha miundombinu ya barabara na inapotokea zinaharibiwa kwa uzembe halikubaliki” amesema.
Homera amesisitiza kuwa wakala wa vipimo washirikiane na Tanroad kuhakikisha wadau wa usafirishaji wanakuwa na elimu ya kutosha kuhusiana na matumizi ya sheria mpya ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya mwaka 2016.
Msimamizi wa mizani kutoka Wizara ya Mawasiliano na Uchukuzi, Mhandisi Leonard Saukwa amesema kuwa lengo la kuwakutanisha wadau wa usafirishaji ni kutoa elimu ya mtumizi sahihi ya miundombinu ya barabara pasipo kuzindisha uzito.